Monday, June 05, 2006

wapo wanasi-hasa wengi tu wakibongo ambao wakiisha wekewa maikrofoni mbele ya midomo yao, basi. kwao, time inakuwa sio money tena...!

siku ya May Day mheshimiwa aliliona hili na kwa vile yeye huwa hakopeshagi, akalizungumzia kwa kuwaambia wanasi-hasa hawa.....



‘Sio lazima kila mtu aongee, jamani'...!

Naam, siku ile ya jumatatu ya wiki hii ambayo ilikuwa ni siku ya watumwa duniani, nikawa nimekaa mbele ya kijiredio changu cha mwaka 47 ili kusikiliza kile ambacho mkuu wa nchi alikuwa anataka kukisema.

Naomba kwanza nisisitize kusema kwamba sina kawaida ya kusikiliza redio kwa mantiki kwamba kuna faida gani kutumia masikio peke yake kusikiliza kitu ambacho Kumbe unaweza pia kukiona kwa macho kupitia kwenye kioo a.k.a tiivii.

Kwa Bahati mbaya, safari hii vituo vyote vya tiivii vikawa havina mpango wa kuonyesha live kile kilichokuwa kikiendelea Shinyanga, mji ambao tangia muandika katikati ya mistari alipouondoka mwaka 1977 akiwa denti wa pale Shaibushi ni kama alikung’uta mavumbi, chembilecho vitabu vya dini, maana mpaka leo hii hajaingiza mguu tena!

Haya basi, ili kupata live hotuba ya mheshimiwa tukalazimika kukumbuka viredio vyetu ambavyo wengine tuliisha vifungasha zamani tukingoja mtu anayekwenda kijijini awapelekee ndugu na jamaa zetu nao wajidai. ganda la muwa la jana ni kivuno kwa chungu.

Kama nilivyokwisha sema. Sina kawaida ya kusikiliza redio hasa ukichukulia kuwa nyingi ya redio zetu zinazosikika vyema siku hizi ni madebe masaa ishirini na tano. Kilichonisukuma kusikiliza redio siku ile ilikuwa ni kutaka tu kujua iwapo iwapo Mheshimiwa ataongeza chochote kitu kwenye masihara yetu ya mshahara, basi.

Nikanunua betri mpya na kisha nikakaa kusikiliza kilichokuwa kikiendelea kule Shinyanga. Waheshimiwa wakaanza kukaribishana jukwaani kuhutubia kwa staili yao ile ile ya miaka nenda rudi tangia mwaka 47aa ambayo sio ngeni sana kwetu…

Mheshimiwa huyu anamkaribisha yule ili amkaribishe huyo ambaye atamkaribisha huyu ambaye atashukuru kwa kupewa nafasi ya kumkaribisha huyu ambaye atazungumza maneno machache (yanayoishia kuwa rundo!) ya kumkaribisha yule ambaye atamkaribisha wa kumkaribisha huyu, ilimradi Kizunguzungu kitupu!

Ni kwa utaratibu huu ndio maana masaa kadhaa baadaye, muandika katikati ya mistari akawa hajamsikia yule ambaye alikuwa amemfanya aibue kiredio chake huko kilikokuwa na anunue betri mpya ili kumsikiliza.

Mwandika katikati ya mistari akajiuliza iwapo waheshimiwa wale waliokuwa wakiendelea kupokezana vijiti vya kukaribishana walikuwa kweli hawafahamu kuwa watu walikuwa wamejaa uwanjani pale kumsikiliza mheshimiwa na sio mtu mwingine yoyote.

kwamba wengine, kama huyu Chizi, walikuwa wamelazimika hata kuibua viredio vyao vya zamani kutoka walikokuwa wamevichimbia ili tu kusikia live kitakachosemwa na Mheshimiwa badala ya kutegemea RedioMbao FM!

Kwa hakika, muandika katikati ya mistari hakuona umuhimu wa kuanza kusomeshwa historia ya vyama vya wafanyakazi pale maana ameishahudhuria siku za wafanyakazi kama thelathini mfululizo kwa kwenda nyuma na kila siku yanayosemwa ni yale yale tu na anaweza kuyakariri hata kwa kinyume nyume!

Haya, unaambiwa stepu fulani pia tukachomekewa ratiba ya kuzawadia wanamichezo. Mwandika katikati ya mistari akajiuliza mno. Ile ilikuwa ni sikukuu ya wafanyakazi, wafukuza upepo na wacheza mpira walikuwa wapi na wapi pale, potelea mbali kwamba nao pia walikuwa wafanyakazi!

Ndio, kwa nini zawadi zao kwa washindi zisingekabidhiwa jana yake na siku ile wakatuacha tuendelee na programu nyingine? Ina maana tulitakiwa tutegemee sasa kwamba siku ya kuzawadia wanamichezo bora wa mwaka basi watazawadiwa pia dakitari bora wa mwaka, mwalimu bora wa mwaka na pengine hata mpiga debe bora wa mwaka?

Jamani wabongo, mbona tunapenda kuchanganya mambo hivi? Si ndio haya haya ya ile shughuli ya klabu bingwa ya warembo nchini kuchukua zaidi ya masaa matano hadi saba na pengine mpaka alfajiri wakati ile ya dunia inachukua masaa mawili tu?

Hatimaaaaaye, wakati huyu muandika katikati ya mistari akiwa ameishaanza kusinzia kwenye kochi ndipo watu wakakumbuka kuwa ala, Kumbe Mheshimiwa naye anatakiwa kuhutubia na hivyo kumualika jukwaani.

Nnachompendea huyu Mheshimiwa ni kutokukopesha maneno. Utafikiri ni mdau wa ‘katikati ya mistari’. Bila kuuma uma maneno cha kwanza alichotamka kikawa kile kile kilichokuwa kichwani mwa Chizi, kwamba siri moja ya shughuli kama zile ilikuwa ni ile ya kuamua kuwa sio lazima kila mtu azungumze!

Kwamba kulikuwa hakuna ulazima wowote wa kusoma kila salamu iliyotumwa kuanzia mwanzo hadi mwisho kwani ingetosha tu kusema kuwa tumepokea salamu kutoka kwa huyu na huyu na yule basi, bila kuanza kuzisoma zote! Makofi, tafadhali!

Kwamba hatari kuu ya kutaka kila mtu jukwaani azungumze ilikuwa ni ile ya kujikuta waheshimiwa mlioko jukwaani mko peke yenu na mnahutubiana wenyewe kwa wenyewe maana kila mwananchi ameishachoka na kuishia zake.

Kwa kifupi kabisa, ujumbe wa Mheshimiwa kwa waheshimiwa wale ulikuwa ni kukumbuka kuwa ‘time is money’. Kwamba kulikuwa kuna taratibu nyingine ambazo kwa hakika kwa karne tuliyonayo hazikuwa za lazima sana kuzifanya.

Kama tumemualika Mheshimiwa kuhutubia May day, basi na tumpe nafasi ya kufanya hivyo. salamu kibao na kuwazawadia wanariadha kwanza nako kunatoka wapi. Time is money, jamani.
chesimpilipili

wakati akina sisi bado tunapoteza muda kwenye mazungumzo, mikakati, mipango na maandalizi ya kutwaa kilicho chetu, wenzetu wanafanya kweli. ndio maana nikauliza.........


Wao wanaweza wana nini ?

Kuna huyu mheshimiwa mmoja kutoka katika nchi iliyopo eneo la Amerika ya kusini ambaye, kama alivyo huyu mheshimiwa mwingine kutoka hii nchi iliyopo mashariki mwa bara la Afrika, ndio kwanzaa amekabidhiwa uongozi wa nchi na wananchi wake.

Ni ajabu kwamba waandishi wa habari wa nchi hii iliyopo mashariki kabisa mwa bara la Afrika hawajasema kuwa mheshimiwa wao amepewa ulaji na wananchi kama wanavyo kimbiliaga kusema pale mtu anapoteuliwa kushika nafasi fulani muhimu ya uongozi. thubutu yao.

Turudi kwa huyu mheshimiwa wa nchi iliyopo Marekani ya kusini. huyu, tumeambiwa kuwa ni mheshimiwa wa kwanza kuongoza nchi hiyo akitokea kwenye kabila la aina fulani ya maponjoro ambalo katika nchi hiyo ni watu wa ngai ya chini kabisa.

Haya, mheshimiwa akatwaa ubingwa wa klabu bingwa ya kugombea uraisi wa nchi nchini humo. akaanza kuweka mambo sawa ambayo kabla ya hapo alikuwa anaona kuwa yalikuwa yakiendeshwa ndivyo sivyo. naam, kama afanyavyo sasa huyu mwenzake wa nchi iliyopo mashariki kabisa mwa Afrika mashariki.

Miongoni mwa rasilimali kubwa ambazo nchi hiyo ya Amerika kusini ilikuwa imebarikiwa kuwa navyo ni utajiri mkubwa wa mafuta. tunalazimika kuharakisha kufafanua mapema kuwa hapa tuna maana ya mafuta ya Petroli, maana kuna watu wakisikia tu mafuta mawazo yao yanakimbilia kwenye Chipsi!

Ndio, nchi hiyo ilikuwa na utajiri mkubwa wa mafuta, lakini kama ilivyo kwa nchi nyenza iliyopo mashariki mwa Afrika mashariki ambayo katika mambo ya railimali kutoka ardhini nayo wamo, mapato yatokanayo na rasimali hiyo waliyopangiwa na Mungu mwenyewe yalikuwa yanawanufaisha zaidi wachache kutoka nje ya nchi wakisaidiana na wachache wengine walio ndani ya nchi.

Mheshimiwa huyu wa nchi iliyopo kusini mwa Amerika akaamua kulifanyia kazi hili kwanza. asubuhi moja isiyokuwa na jina mwezi uliopita akaamka na bila kuuma uma maneno akatamka kwa kujiamini kabisa kuwa kuanzia siku ile visima vyote vya mafuta vitakuwa chini ya usimamizi wa serikali, nani anabisha.

Kama ilivyotegemewa, wakubwa wa dunia ambao ndio makampuni yao yalikuwa yamejazana huko yakichimba mafuta wkaja juu. wakakemea, wakafoka, wakatisha, wakanuna, wakachimba mkwara na kadhalika na kadhalika lakini wapi. mheshimiwa akashika uzi ule ule huku akiwaambia jamaa hapa hakieleweki mpaka kieleweke.

Halafu akatamka maneno ambayo yalimkuna mno muandika katikati ya mistari na kumfanya kuanzia wakati huo atamani sana kuyasikia yakitamkwa na watu fulani mahali fulani kwamba:

'kwa muda mrefu mapato ya rasilimali zetu yamekuwa yakiwanufaisha wajanja wachache badala ya wananchi wenye nchi yao lakini kuanzia wakati huo alikuwa ameamua kusimama kidete ili kuhakikisha kuwa wananchi wake wanafaidika na rasilimali waliyoachiwa na Mungu!'

Naam, maneno mazito kabisa haya ambayo haraka haraka yakaungwa mkono na huyu mheshimiwa mwingine kiongozi wa nchi jirani na huyu mheshimiwa wa kwanza na ambaye ana usongo mno na huyu raisi wa dunia, mheshimiwa Joji Bushi, kiasi kwamba aliisha wahi kusimama kadamnasini na kumuambia Joji lione kwanza, wee si mlevi tuu!

Naam, haya ni maneno ambayo kwa namna moja ama nyingine yalikuwa pia yameishatamkwa na waheshimiwa ambao ndio kwanzaa walikuwa wametwaa uongozi wa nchi njema iliyoko mashariki kabisa mwa Afrika mashariki.

Tofauti ilikuwa ni kwamba mheshimiwa wa nchi iliyo Amerika ya kusini alikuwa amekwenda hatua moja mbele kwa kuyaambatanisha maneno yake na vitendo ambavyo bila shaka aliamini kuwa vitwasaidia wananchi wake huku hawa waheshimiwa wa nchi iliyo mashariki ya Afrika mashariki wakiwa bado kwenye hatua za mazungumzo tu na wanaochimba nchi yao.

Naam, mazungumzo ya kuangalia uwezekano wa mkakati wa kuwezesha nchi ipate zaidi ya Marahaba tatu ipatazo sasa kutoka kwa wachimbaji wa rasilimali zetu ambao wao hupata Marahaba Tisaini na saba kutoka katika kila Shikamoo mia moja zinazochimbuliwa kutoka kwenye ardhi yetu. mwenye masikio na asikie.

halafu kama vile hili sio wazimu tosha, majuzi tumesoma taarifa kuwa hata katika hizo Marahaba tatu tunazopata, kuna kijikampuni fulani cha wenyewe ambacho kinachukua nusu ya Marahaba tatu tunazogaiwa na wakubwa, yaani Marahaba moja na nusu, kwa ajili ya eti sijui kuoditi, ile nusu nyingine ya Marahaba iliyobaki! hili ni jambo linaloweza kutokea Bongo tu.

Inapofika hapa, muandika katikati ya mistari anajikuta akimkumbuka mno yule mzee wetu wa Zimbabwe ambaye naye aliamka tu asubuhi moja na kuamua kuwa kuanzia asubuhi ile mashamba yote yenye rutuba yaliyokuwa yamehodhiwa na wachache sasa yatakuwa chini ya usimamizi wa serikali.

Yamesemwa mengi. ya kumuunga mkono na ya kumponda mzee wa watu. lakini mpaka majuzi mzee alikuwa ameshikilia uzi ule ule ingawaje alikuwa tayari ameishaulegeza kidogo wa kuwataka wanaotaka kurudi kwenye mashamba yao wafanye hivyo ingawaje kwa sasa ni kwa taratibu mpya zinazokidhi mahitaji ya wananchi.

Mwandika katikati ya mistari hapa hatataka kuzungumza kuhusu yule mheshimiwa Dada wa nchi ya jirani ambaye naye siku moja aliamka asubuhi na kuamua kuwa ili wananchi wake wapate faraja basi wahindi wote, out! huyu tumuache maana, amin amin nawaambia, alikwisha kupata thawabu yake.

Mwandika katikati ya mistari anadhani kwamba ni lazima na sisi tufike mahali asubuhi moja tuamke na na kuamua kuwa kuanzia asubuhi hiyo mashimo yoote yanayochimbwa rasilimali zetu sasa yapo chini ya usimamizi wa serikali hadi tutakapopanga taratibu nyingine, full stop.

Na kwa hili hatuna haja ya kumuigiza mtu maana tayari tuna ozoefu nalo. ndio, asubuhi moja ya mwaka 1967 mheshimiwa mmoja ambaye sasa ni marehemu aliamka na bila kujiuma uma wala kutafuta suluhu na mtu alitamka wazi kabisa kuwa kuanzia siku ile mabenki na majumba yoote makubwa yangekuwa sasa chini ya usimamizi wa serikali, nani anabisha.

Hakuna aliyethubutu kubisha. ndio maana muandika katikati ya mistari anadhani wakati umefika sasa wa kujiuluza kama walivyojiuliza wadogo zake fulani....kwani wao wanaweza wana nini hadi sisi tushindwe tuna nini? alamsik.