Monday, May 15, 2006

chesimpilipili

kweli haya mambo bado ni mageni kwa tulio wengi. hapa nilitaka kuwawekea picha moja kuonyesha jinsi ninavyoachia mdomo wakati ninapotafuta cha kuandika. katika kuminya huku na kule, nikashitukia zimetoka mbili tena sio pale nilipotaka zitokee. maana mimi nilitaka itoke moja tu ndogo hapo kwenye 'about me'. matokeo yae ndio haya. kweli, ndesyanjo bado ana kazi.......!!

Friday, May 05, 2006

chesimpilipili

Wakati kheshimiwa mpya wa Bongo alipotimiza siku mia moja ofisini, kila mtu aliandika makala. mimi niliamua kungoja hadi siku kumi baadaya ndio nikaandika hii niliyoiita...

Siku 110 ofisini...!



Alhamisi ileee, kama siku hivi kumi zilizopita, wakati hii awamu ya nne ya uongozi wa nchi njema ya Bongo inatimiza siku mia moja, tulishuhudia jinsi kila aliyekuwa anajua kuandika alivyochongoa kalamu yake na kuchonga.

Napenda kuamini kuwa maneno haya ni ya kistaarabu zaidi kuliko kama ningesema kuwa kila mwenye mdomo aliuchongoa na kuchonga.

Naam, siku ile ya Alhamisi wakati awamu ya nne ya uongozi inatimiza siku mia moja ofisini kila mwenye kalamu yake aliishika na kuandika kile alichoamini kuwa ni bonge ya makala.

Zilikuwa makala za kusisimua mno kiasi kwamba ungedhani watu wanasherehekea kutimiza miaka mia moja ya uongozi na kumbe ni SIKU mia moja tu!

Mwandika katikati ya mistari hataki kuamini kwamba siku mia moja zinatosha katika kukupa muelekeo wa jambo fulani.

Pengine ndio maana akaamua kuacha kitim tim cha kuandika kuhusu siku mia moja kitulie kwanza ndipo na yeye atie neno lake. maana wote tungeandika wakati ule sijui nani angemsoma mwenziwe.

Kikubwa alichogundua mwandika katikati ya mistari katika kitim tim kile ni kuwa nchi njema ya Bongo haina uhaba wa wafagiliaji na eeee, kidedea.

Wapo wa kumwaga. kulikuwa na makala nyingi zaidi za kufagilia kuliko zilizokuwa na alama za kuuliza.

Si nia ya muandika katikati ya mistari kuingilia uhuru wa mtu kutoa maoni yake. na ndio maana hata yeye hategemei mtu kuanza kumuona kuwa si mwenzetu kwa vile tu makala yake itakuwa imejaa maswali mengi zaidi kuliko mafagio. ndio, wenzake weengi wameishafagilia. yeye anaomba kuzungumzia zaidi upande wa pili wa gwala.

Haya, siku mia na kumi. kikubwa alichoona huyu last born wa marehemu mzee Mpilipili katika kipindi hiki cha siku mia moja na kumi ni maagizo, maelekezo na maonyo meengi ambayo wakati fulani yalianza kumfanya aone kama tulikuwa tumerudi tulikotoka. maagizo na maelekezo kibao yaliyokuwa na muelekeo wa kuishia kuwa hivyo hivyo, maagizo na maelekezo tu.

Anadhani kwamba waheshimiwa wa awamu ya nne walikuwa wanaenda kasi mno kiasi cha kutuacha sisi wengine wote nyuma. waama, Chesi anadhani kwamba sio vibaya iwapo waheshimiwa hawa wakasimama kidogo kutusubiri na pia kufuatilia kama yale maagizo na maelekezo yote wanayotoa huku nyuma yanatekelezwa.

Kuna hili la sirikali kuanza na migulu baja kwenye suala kubwa la kubana matumizi yake. tumeshuhudia tumizi kubwa la waheshimiwa walioteuliwa kuja Dizim na kuishi kwenye hoteli za bei mbaya wakisubiri nyumba, ushahidi kamili kwamba uamuzi wa kuuza nyumba za taifa kwa watu wawili watatu ni mchemsho wa karne, ingawaje nafasi bado ipo ya kulirekebisha hili kwa kurudisha nyumba zile kwa wananchi na kuwarudishia chao waliozinunua.

Basi waheshimiwa wenyewe waje peke yao, aa wapi. wengine walikuja na wake zao, na watoto wao na labda hata vijukuu na hivyo badala ya mheshimiwa kuchukua chumba kimoja tu katika hoteli ya bei mbaya, anachukua vitatu. cha kwake na mamaaa, cha watoto na sebule, maana wageni anaomtembelea mhishimiwa hawawezi wakaingia chumbani kwake moja kwa moja wasije wakaona deshi deshi zake zimeanikwa kwenye tendegu la kitanda!

Naam, hii ni tofauti iliyoje na pale huyu Chesi alipohamishiwa Darisalama mara ya kwanza miaka hiyoo ya 47 ambapo ili kubana matumizi alilazimika kutangulia yeye na bi mkubwa kwanza na kuishi kwenye kijigesti fulani cha uchochoroni hadi pale alipopata makazi ndipo aliporusu umati wake wote kutia timu jijini!

Muandika katikati ya mistari anatamani mno kuwa badala ya kugharamiwa na sirikali, kila mmoja katika waheshimiwa hawa angekatiwa kabisa posho yake ya safari na manaiti yake kama anavyofanyiwa yeye anapobahatisha kwenda safari, kisha tuone. thubutu kama mtu angekaa kwenye hoteli ya bei mbaya na kadamnasi yake!

Haya, katika siku mia moja na kumi tumemsikia pia mheshimiwa wetu akitamka bayana kuwa ana majina ya wala rushwa wote lakini anawapa muda kwanza ili kujirekebisha. hii ni kauli iliyomkumbusha sana mwandika katikati ya mstari juu ya kauli fulani ya hapo zamani za kale juu ya kwamba wala rushwa wote wangekiona cha mtema kuni lakini baadaye ikabadilika na kuwa ya kutaka ushahidi kwanza kabla ya cha mtema kuni!

Hawa watu wameishaitafuna sana kama mchwa nchi yetu njema hii ya Bongo. kuwapa tena muda wamalizie malizie kuitafuna haimuingii akilini muandika katikati ya mistari. hawa kwa hakika ni watu waliostahili kufanyiziwa kwa kasi ile ile iliyotumika kuwatoa mkuku wagonga kokoto kule kwenye machimbo yao ama wenye vibanda vyao katikati ya jiji. staili ya hakuna cha mswalie mtume!

Ndio, ili kuepusha kuonekana ni ' yale yale', kasi mpya inapaswa kuwa ni upanga wenye makali ya kukata kote kote badala ya kuwa na ukali wa ajabu pale tu inapokuwa ni suala la kuvunja vibanda vya Big Brother Manzese, lakini inapokuwa ni suala la kukata manyangumi na mapapa wala rushwa ghafla unakuwa butu na kuanza kusua sua!

Katika siku mia moja na kumi hizi pia tukaambiwa kukaa standby kusikiliza orodha ya majina ya wale walioaminika kuwa ni majambazi makubwa. muandika katikati ya mistari na walala hoi wenzake wakakaa mkao wa kula wakisubiri mijina mikubwa mikubwa ya mijambazi iliyokuwa inaivuruga Bongo yetu njema hii.

Jiji jema la Dizim likatangaza kile kilichosemekana kwamba ni majina ya mijambazi mikubwa mikubwa na muandika katikati ya mistari akajikuta akishindwa kuzua muayo wake. hakuna jina lolote lililoshitua mtu na kwa hakika muandika katikati ya mistari hatashangaa sana iwapo miongoni mwa orodha ile kutakuwa na wauza karanga wawili watatu. Hivi watu wanajua maana ya majambazi wakubwa kweli?

Ni kweli, yalikuwepo majina mawili matatu yaliyoshitua watu kiasi fulani lakini watajwa walipofikishwa mahakamani wakiwa wametinga magold na masuti yao huku wakitabasamu muandika katikati ya mistari akakata tamaa na kuona kama ni aina fulani ya mchezo wa kuigiza hasa pale anapokumbuka kuwa wadogo zake wanapofikishwa 'kaunta' (kama unadhani ni ya Bar, pole!) huamrishwa kuvua kila kinachoweza kuvuliwa, na kama huna bahati hata nywele!

Hapo hapo kwenye orodha ya majina tukaambiwa kuwa tungetajiwa pia orodha ya majina ya askari wa vyeo vya juu ambao walikuwa wakishirikiana na majambazi. tukasubiri, tukasubiri, tukasubiri wee. wakatajwa wawili watatu wenye vyeo ambavyo sio kitu cha kuandikia barua nyumbani kisha, kimya.
habari iliyokuwa ukurasa wa mbele sasa imeishia kuwa ya ukurasa wa matangazo...!

Ni mambo kama haya ambayo yanamfanya muandika katikati ya mistari aombe kwanza kuweka fagio lake mfukoni. ni mpaka hapo atakapoona mtu mzima ananyolewa nywele kwa kigae cha chupa ndipo labda, laabda atalitoa na kufagilia mtu. Asalaam aleikum.
chesimpilipili

hii niliiandika wakati nchi yetu njema ya Bongo inatimiza miaka 41 tangia tupate uhuru......


tuwaite, waje kuona ... ?

Mwandika hekaya alikuwa dogo wa miaka kumi na mbili tu na akisoma darasa la nne hapo katika shule ya msingi ya Chang'ombe wakati nchi njema hii ya bongo ikisherehekea miaka kumi ya uhuru wake pale mwaka na 1971.

Anakumbuka mno jinsi yeye binafsi alivyoshiriki kikamilifu katika sherehe hizo kwa kuwa miongoni mwa mamia ya wanafunzi wa shule za msingi na sekondari za jiji jema la Dizim walioshiriki katika maonyesho kabambe ya halaiki yaliyofanyika pale uwanja wa taifa.

Naam, maonyesho ya halaiki ambayo mpaka leo hii wachokozi wa mambo bado wanakubaliana kwamba hayajapata kutokea tena mfano wake, pengine kutokana na ukweli kwamba ilifundishwa na waalimu wa kichina orijino kutoka china!

Haya, mwandika hekaya pia anakumbuka mno nyimbo kadhaa za muziki wa dansi zilizotungwa na wasanii wetu kwa ajili ya kipindi cha sherehe hizo.

Anakumbuka mno ule wa bendi marehemu ya Urafiki jazz, wakati huo ikiongozwa na mzee Mrisho, Ngulimba wa Ngulimba, wimbo ambao pamoja na mambo mengine, ulielezea mafanikio yaliyokuwa yamepatikana katika kipindi hicho cha miaka kumi ya uhuru.

Ikatajwa reli ya Tazara, chuo chetu kikuu, vyama vyetu vya ushirika, jeshi letu la mgambo( wakati huo likiwa jeshi la mgambo kweli na sio haya masulupwete tunayoshuhudia siku hizi!) na hata kisomo cha watu wazima kikatajwa kama moja ya mafanikio yetu!

Haya, mwandika hekaya pia akakumbuka mwimbo mwingine uliokuwa umeimbwa na hayati Mbaraka Mwishehe Mwaruka ambao ulielezea jinsi wakoloni walivyokuwa wametuchelewesha na hatua ambayo tulikuwa tumeifikia baada ya wao kung'atuka.

Lakini, zaidi mno muandishi wa hekaya anakumbuka mno wimbo ulioimbwa na Nuta jazz, kama hajakosea sana, ambao maneno yake anayakumbuka vizuri mpaka leo hii:

'sasa tutawaita waje kuona wenyewe,

hatutafanya kitu tukashindwa,

sasa tutawaita waje kuona wenyewe,

maendeleo yetu yanakwenda vyema....'



Naam, mwandika hekaya hana uhakika sawa sawa, lakini anadhani kwamba maneno ya wimbo huu yalikuwa yametokana na hotuba moja ya raisi wa nchi wa wakati huo, mwalimu Julius Nyerere, ambapo alikuwa amesema kwamba tungewaita wale waliotutawala waje kuona tulipokuwa tumefika katika kipindi cha miaka kumi.

Na kwa hakika wakati huo tulikuwa kweli na jeuri ya kuweza kuwaita waliotutawala na kudai kwamba tulikuwa bado kustahili uhuru, waje kuona mambo makubwa tuliyokuwa tumefanya katika kipindi hicho cha miaka kumi. ndio, tulikuwa na jeuri hio!

Ukiachilia mbali mambo makubwa kama yale ya ujenzi wa chuo kikuu, viwanda kama kile cha nguo cha Urafiki,na Mwatex na cha zana za kilimo cha Ufi na kadhalika na kadhalika, nchi hii ilikuwa imepiga hatua kubwa mno katika huduma za jamii.

Huyu muandishi wa hekaya anakumbuka mno kwamba katika kipindi hicho alikuwa akiishi na shemeji yake mmoja pale Chang'ombe mtaa wa Ngorogoro nyumba namba 98, na anakumbuka mno pia kwamba hakupata kushuhudia kitu kinachoitwa kukatika umeme ama maji kukatika kwa siku tatu nzima, never!

Kila mara muandika hekaya anapowahadithia haya wanawe, huishia kuona huruma jinsi wanawe wanavyobaki kung'aa macho kutoana na mshangao kwa vile wao katika kipindi hiki cha mgawo, umeme huja saa tano usiku na 'kuondoka'
saa kumi na mbili alfajiri!

Anakumbuka pia mno jinsi mitaa ya Magomeni, Ilala na kwingineko ilivyokuwa misafi ikiwa na lami, mbali na kila nyumba kuwa na pipa lake la takataka ambalo lilikuwa likija kuchukuliwa takataka zake na gari la site kila baada ya siku mbili!

Siku hizi ukiweka pipa la taka nje kesho hulikuti maana unakuwa umewapa watu kifaa cha kuhifadhia maji kutokana na maji kuwa ya mgawo!

Na hapa chesi anaogopa hata kudokeza kwamba yeye alisoma darasa la pili hadi la sita katika shule hio ya msingi ya Chang'ombe akiwa amekalia dawati lake la mtu mmoja mmoja tu, sio watatu, kwa kuchelea kwamba watu hawatamuamini, kwa vile hata watoto ake tu wanadhani anayowaambia ni fiksi zake tu!

Ni wazi basi kwamba baada ya wabongo walio wengi kushuhudia mafanikio haya ya miaka kumi, walitegemea kwamba hadi nchi hii itakapofikia miaka thelathini ama arobaini ya uhuru, ingekuwa pungufu kidogo tu ya peponi! ole wao. ole wetu.

Muandika hekaya angependa kuwahoji wabongo wenzake. ni kweli kwamba katika kipindi hiki wakati nchi njema ya bongo inasherehekea kutimiza miaka arobaini na moja ya uhuru wake, tunayo jeuri ya kuwaita waliotutawala waje kuona mafanikio yetu, kama alivyofanya baba wa Taifa wakati wa kusherehekea miaka kumi ya uhuru wetu mwaka na 1971??

Tuwaite? waje kuona nini? barabara za katikati ya jiji walizoziacha na lami na ambazo sasa baada ya miaka 40 ya Uhuru ni vumbi tupu, hata zile za kwao akina chesi kule Bumbuli zina nafuu?

Waje kuona nini? bomba kuu kukuu la kuleta maji jijini ambalo toka waondoke wao hakuna mtu ambaye ameishapata angalau kuwaza kutafuta vyanzo vingine vya maji badala ya waheshimiwa kila mara kujazana mahali bomba linapopasuka na kuahidi wananchi kwamba maji yatatoka baada ya siku mbili tatu!!

Tuwaite waje kuona nini? hospitali zisizokuwa na dawa? shule zisizokuwa na madawati? nyumba za watumishi wa serikali walizoziacha ambazo sasa kwa kisingizio cha sirikali kushindwa kuzimeintein, sasa zinapigwa bei kama nguo za mitumbani?

Mwandika hekaya anaweza kuandika mengi lakini lililo wazi ni kwamba, pamoja na kwamba kuna watu watabisha, yeye haoni kama tunao ubavu wa kuwaita walee waliotuwala ili waje kuona maendeleo yetu baada ya miaka AROBAINI NA MOJA ya uhuru wetu! alamsik.