Friday, August 24, 2007

Kuna maamuzi yanayopitishwa na waheshimiwa ambayo yanakufanya mtu ujiulize iwapo nchi hii ina wenyewe. Kama hili la wafanya biashara 'waaminifu' kuruhusiwa kupitisha mizigo yao bandarini chap chap bila kukaguliwa. Ndio maana nikalikejeli...

'Nyungo' mbili kubwa zilizo kichwani mwa huyu muandika katikati ya mistari ambazo pia hujulikana kama masikio zimedaka taarifa muhimu kuhusu wafanya biashara wa nchi njema ya Bongo ambazo zimemsisimua mno mmiliki wa 'nyungo' hizo.

Hizi ni zile taarifa zilizotangazwa majuzi na waheshimiwa wetu kuwa kuanzia tarehe fulani huko mbele wafanya biashara ‘waaminifu’ wataruhusiwa kupitisha mzigo yao pale bandarini chap chap bila kukaguliwa, wakauze wanachouza kisha baadae wao wenyewe waseme walipitisha nini na wanapaswa kulipa nini!

Yapo mambo ambayo muandika katikati ya mistari husisimka mno anapoyasikia.Hili ni mojawapo. Hii ni pamoja na kujijazia maujiko kila mara kwamba ngozi yake imeshakuwa sugu na politiki za nchi njema ya bongo kiasi kwamba hakuna kinachoweza kumsisimua tena kutoka kwa wanene wa nchi.

Kwamba ati kuanzia tarehe fulani huko mbele ya safari wanaosemekana kuwa wafanya biashara waaminifu wa Bongo wataruhusiwa kupitisha bandarini chap chap lumbesa, magunia, maboksi, matenga na makontena yao bila kuulizwa na mtu kilichomo.

Kwamba baada ya kupitisha mizigo yao bila kulazimika kueleza kilichomo wataenda kuuza kilichomo kisha watarudi kunako husika na kulipa wanachotakiwa kulipa kutokana na walichouza!

Wafanya biashara waaminifu! Kwanza muandika katikati ya mistari anashituka na kushangaa kuwa maneno haya mawili ‘wafanya biashara waaminifu’ bado yapo kwenye msamiati wa lugha yetu njema ya Kiswahili. Wafanya biashara waaminifu! Bongo hii??

Muandika katikati ya mistari anapata tabu mno kuamini kuwa ndani ya Bongo yetu njema hii katika karne hii bado kuna kabila la watu linaloitwa ‘wafanya biashara waaminifu’. Kwa hakika, ni wale wenye roho ya Paka tu, ambao wanaweza kuamini uwepo wa kabila hilo!

Kwamba bado tunao wafanya biashara ambao ni waaminifu vya kutosha kiasi kwamba tunaweza kuwaruhusu kupitisha vijikontena vyao viwili vitatu bila kulazimika kutuambia kilichomo, wakaenda kuuza kisha wakarudi na kutuambia wameuza nini na kulipa wanachopaswa kulipa kama kodi kutokana na mauzo yao!

Kuna mtu mahali anataka kufanya mzaha mbaya. Huu wa kuwaruhusu wafanya biashara wanaosemekana kuwa ni waaminifu kupitisha mizigo bandarini bila kukaguliwa, wakauze kisha ndipo warudi kulipa kodi inayotakiwa ni mzaha mbaya hata kwa nchi iliyobobea katika mizaha kama Bongo!

Muandika katikati ya mistari anajiuliza mno iwapo hapa waheshimiwa walikuwa wanazungumzia Mitume ama Watawa fulani hivi ama tulikuwa tunazungumzia wafanya biashara dizaini ya Rada ama wale wa mashine za umeme za kufua giza badala ya kufua mwanga!

Wafanyabiashara waaminifu? Wepi? Hawa tusioisha kuwasoma kwenye magazeti wakikopeshana na kuchezea akiba ya uzeeni ya Chesi kwa kununua, kukarabati na kisha kuyapiga bei mbaya magofu kadha wa kadha huku Chesi mwenye akiba yake akikosa hata haki tu ya kukopa akiba yake mwenyewe!

Ndio, wafanya biashara waaminifu wepi? Hawa hawa wanaopita mlango wa nyuma kupewa mikopo inayogeuka makopo ya chooni baada ya siagi iliyokuwemo kuliwa?

Kwa hakika, muandika katikati ya mistari anasubiri kwa hamu mno kutangazwa kwa vigezo vya mfanyabiashara muaminifu ili na yeye atie timu na kuuagiza kijikontena chake chenye vijenereta alfu mbili ambavyo kutokana na sifa ya uaminifu, vitapita pale bandarini chap chap bila kukaguliwa!

Ni utume na utawa, ambao hana, ama uwendawazimu tu utakaomfanya Chesi arudi kunakohusika baada ya mauzo yake na kwa akili zake timamu kabisa aseme kweli kwamba kijikontena chake kilikuwa na vijenereta alfu mbili na kodi yake hii hapa!

Bongo haiishiwi na mapya yanayokufanya ujiulize mara mbili mbili juu ya utashi wa baadhi ya watu. Hili ni mojawapo. Tutafakari.



Hakuna kitu kinachowaumiza wazazi kama wakati wa wanafunzi kurudi shule baada ya likizo unapowadia. Ni kasheshe tupu. Nikaona niliandikie hili....

Binti wa mama yangu mdogo amefaulu kwenda shule ya sekondari kubwa lakini ameniacha nikijiuliza iwapo kweli anakwenda shule ama kambi ya skauti.

Nimeangalia barua yake ya maelezo ya kujiunga na shule husika na vifaa na michango anayotakiwa kuwa nayo na kubaini kuwa kama sio kujiunga na kambi ya skauti basi bila shaka itakuwa ni kuhudhuria kikao cha harusi lakini kamwe sio shule.

Nasema huenda binti ya mama yangu mdomo anakwenda kambi ya skauti kutokana na ukweli kwamba baadhi ya vifaa anavyotakiwa kuwa navyo wakati anajiunga na shule husika havihusiani kabisa na kwa namna yoyote na masomo tunayofahamu ya sekondari.

Nasema pia kuwa huenda binti yetu huyu anakwenda kuhudhuria kikao cha michango ya harusi kwa vile baadhi ya michango kwenye orodha ndeefu ya michango anayotakiwa kuwasilisha shule haihusiani kwa namna yoyote ile na masomo ya kawaida ya sekondari tunayofahamu sisi.

Naangalia kivuli cha barua ya kujiunga na shule husika nilichotumiwa na mama yangu mdogo akiniomba kuangalia ni kipi ninachoweza kuchangia miongoni mwa orodha ndeefu ya vifaa na michango anayotakiwa kuwa nayo binti yetu kabla hajaruhusiwa kukalia dawati la shule.

Bila mzaha, nimemuandikia barua mama yangu mdogo na kumjibu kuwa katika yoote hayo mimi nitachangia kukodisha Fuso pale Jangwani kwa ajili ya kusafirisha binti yetu na rundo lake la vifaa na michango anavyotakiwa kuwasili navyo shule!

Ndio, barua ya kujiunga na shule husika inamtaka binti yetu aende shule na godoro, aende na mto wa kulalia, aende na chandarua, aende na ndoo ya plastiki, aende na sahani na kikombe na kijiko, aende na jembe na aende na kiila kitu ambacho muandika katikati ya mistari anajilazimisha kuamini kuwa kwa namna moja ama nyingine kinahusika na kusoma!

Naam, ndoo, sahani, kijiko na kikombe! Kwa hakika nikashangaa sana kwamba orodha ile haikumalizia kabisa kwa kumtaka aende pia na mwiko na jiko la mchina tukajua moja kuwa alikuwa anakwenda kuanza maisha mapya ya ajira na sio kwenda shule!

Yakafuata yanayohusiana na kusoma. Akatakiwa aende na rundo la madaftari, sare za shule rundo, sare za michezo rundo, viatu na soksi vya masomo na michezo rundo na kadhalika na kadhalika ambavyo ukijumlisha na vile vingine ilikuwa dhahiri kuwa ninalazimika kumkodishia binti yetu usafiri wa Fuso kumbeba yeye na vifaa vyake rundo!

Kukafuata orodha ya michango. Nikadhani kwamba ile ilikuwa ni taarifa ya kamati fulani ya michango ya harusi na kamwe sio barua ya mwanafunzi ya kujiunga na masomo ya shule za sekondari!

Kukawa na mchango wa dawati, mchango wa choo cha shule, mchango wa beji mbili za shule, mchango wa mtambo maalumu wa shule wa kuzuia vibaka, yaani mlinzi, mchango wa matibabu na kadhalika na kadhalika.

Na katika kudhihirisha kuwa kiendacho kwa Mganga hakirudi, barua imefafanua wazi kabisa kuwa hela inayotolewa kama mchango wa matibabu haitarudi hata kama binti yetu atadunda mwaka mzima shuleni hapo bila kuuugua!

Kwa hakika, ilikuwa ni orodha ndeefu ya michango kiasi kwamba nikashangaa ilipofika mwisho bila kuona mchango wa MC, mchango usafiri wa Bwana na Bibi Harusi, mchango wa matarumbeta na mchango unaoendana na chochote kinachohusu sherehe za harusi!

Ndio, ilikuwa ni orodha ndeefu ya michango iliyonifanya nikumbuke mno wakati ulee tulipotakiwa kuchangia timu yetu ya taifa ya vijana na kila mtu kutoa chochote alicho nacho kuanzia Ndoo mbili za suruali, boksi mbili za vitumbua hadi debe mbili za mashuka katika kuitikia wito wa “jamani, isaidieni Serengeti Boys!”

Naam, ilikuwa orodha ndeefu ya michango iliyonifanya nijiulize iwapo binti yetu alikuwa anakwenda shule ama kwenye kikao cha harusi!

Ndio, ilikuwa pia ni orodha ndeefu ya vitu iliyonifanya nijiulize mno ziko wapi zile siku kama za mwaka ulee wa 1974 nilipotoka pale shule ya Msingi Mfaranyaki Songea na kwenda fomu wani kule Musoma Alliance ambacho nilichotakiwa kubeba kilikuwa ni sare za shule tu nilizofungia ndani ya msanduku wangu wa mbao uliokuwa na ziinga la kufuli!

Ndio, kwa hakika nimekuwa nikijiuliza mno juu ya mwanafunzi wa kidato cha tano anayetakiwa kwenda shule na ndoo ya plastiki ambayo ni salamu tosha kwake kuwa kama kwao alikuwa amezoea kuoga maji ya bomba la mvua, basi sasa atatakiwa agawe muda wake katika kusoma na kusaka maji!

Katika yote haya, nimemuandikia mama mdogo barua kuwa ninachoweza kuchangia kwenye hili ni kukodisha Fuso pale Jangwani kwa ajili ya kumsafirisha binti yetu na rundo lake la vifaa anavyotakiwa kuripoti navyo shule!
Sasa tunatafuna nyama kama vile hakuna kesho. lakini siku chache za nyuma, gonjwa baya la Rift Valley Fever, RVF, lilifanya watafuna nyama wote waone nyama kama kituo cha Polisi. katikati ya dhahama hiyo niliandika makala hii...

Muandika katikati ya mistari anakatiza mitaani na kuangalia nyama ya ng’ombe inavyoshangaa shangaa kwenye mabucha kama vile haina mwenyewe na anaishia kujiuliza iwapo ni majuzi tu mambo yote yalipokuwa yeye na nyama, nyama na yeye.

Anaangalia jinsi minofu ya nyama ilivyobakia kuwa maeneo ya kujidai ya nzi badala ya kuwa maeneo ya kujidai ya meno yake na anaishia kujiuliza ni lini kiama hiki cha kuona nyama kama kituo cha Polisi kitakapoishia.

Waama, muandika katikati ya mistari anajiuliza mno juu ya watu hawa waliokuwa mabingwa mno wa kumtangazia na kumtaka kuiona nyama kama kibaka akionavyo kituo cha Polisi ghafla bin vuu kugeuka mabubu linapokuja suala la kumruhusu kukandamiza manyama kwa kwenda mbele.

Kwa hakika, huyu wenu mpendwa haoni aibu kukiri kwamba kama walivyo wanaume wengi wa kibongo linapokuja suala la kula nyama, yeye ni mroho plus.Ndio, kwamba linapokuja suala la supu, mishikaki, utumbo na vitengo vingine vyote vya nyama, yeye ni Simba wa Tsavo.

Ndio, kama ilivyo kwa wanaume wengi wa kibongo, yeye alikuwa ni adui nambari wani wa Ng’ombe na Mbuzi, akiteketeza bila huruma kilo juu ya kilo za nyama za wanyama hao saa ishirini na nne na siku saba za wiki.

Unaambiwa ratiba ilikuwa asubuhi kabla ya kuingia mzigoni ni supu ya ng’ombe ama Mbuzi pale mitaa ya Kisutu, mchana anafakamia wali nyama kwa mama lishe, jioni anaungana na kampani na kwenda kurarua nyama za kuchomwa na mishikaki kabla ya kumalizia nyumbani usiku wali na nyama. Naam, nyama kwa kwenda mbele!

Wakazuka hawa jamaa ambao muandika katikati ya mistari anahisi kwamba walimuona anafaidi sana na hivyo kumfanyia fitna kwa kutangaza kuwa kile alichokuwa akipenda sana kilikuwa kimeingiwa na homa ya bonde la Ufa na sasa kimekuwa tiketi tosha ya kukupeleka maeneo ya juu kwa Muumba wako.

Hakuna apendaye ku-rest in peace bila sababu za msingi. Ghafla bin vuu nyama ikageuka kuwa kituo cha Polisi mdomoni mwa muandika katikati ya mistari na Simba wa Tsavo wenzake!

Badala ya kula nyama ya Ng’ombe muandika katikati ya mistari sasa akajikuta akilazimika kula kilichokuwa chakula cha Ng’ombe, yaani majani. Kuanzia mchicha hadi kabichi hadi kisamvu hadi nyasi nyinginezo! Supu yake sasa ikawa ile ya karoti tupu!

Hapo nyuma kidogo huyu muandika katikati ya mistari alikuwa na kawaida ya kuwashangaa kwa kebehi wala mboga mboga bila nyama waliokuwa wamejipa jina la ‘vejetarian’. Akajikuta yeye sasa akigeuka kuwa vejetarian wa nguvu kuliko hata vejetarian wenyewe orijino!

Naam, kwa siku kadhaa kukawepo na taarifa za kuwataka wakazi wa jiji jema la Dizim kukaa chonjo kwa sababu homa ya ng’ombe ilikuwa hapo Boma la Ng’ombe tu, mara ikawa Dodoma, mara Morogoro, na mara Kibaha.

Kwa hakika, kuna wakati huyu Chesi alikuwa anaona kabisa kuwa magazeti yalikuwa kwenye ushindani usio rasmi wa gazeti lipi litakuwa la kwanza kuandika juu ya ugonjwa huo kuingia jijini!
RVF ikawa kushoto, kulia na katikati.
Muandika katikati ya mistari haoni aibu kukiri kwamba alikuwa akisononeka mno kuona minofu ya nyama ikizagaa zagaa tu kwenye bucha huku wanaozifaidi wakiwa mainzi tu!

Siku kadhaa baadaye muandika katikati ya mistari na waroho wa nyama wenzake anashuhudia kupungua kwa kiasi kikubwa kwa taarifa muhimu juu ya RVF. Anashangaa kuona hata ule ushindani wa vyombo vya habari wa kuandika juu ya ugonjwa huo unavyosogelea jijini ukiwa umepungua mno, kama sio kwisha kabisa.

Pamoja na upungufu huu wa taarifa za ugonjwa huo, bado muandika katikati ya mistari hajapata ujasiri wa kusimama mbele ya Bucha na kumtaka muuza nyama akamtie kiuno na kukichukua kiuno hicho hadi nyumbani kwa ajili ya kitoweo.

Naam, ameishia kuwaonea donge majasiri wanaomhadithia kuwa jana walinunua nyama na kuigagadua tani yao bila kujali cha RVF wala nini! na donge linazidi zaidi pale anapoona wagagaduaji hao wakiendelea kudunda bila hata hata dalili ya kuugua angalau kamalaria ama kamafua tu! laiti na yeye angekuwa na ujasiri huu!

Anashindwa kujidai na hilo kwa sababu hakuna mhusika yoyote miongoni mwa wale waliojitokeza kwa nguvu zao zote kumchimbia mkwara kuhusu RVF ambaye ameishajitokeza hadi sasa kutamka kuwa tishio limeishapungua hivyo mwenye kutaka kula nyama,aale. Anayetaka kula utumbo, aale. Anayetaka kukatiwa kiuno, na akatiwee!

Ndio, ni kwa vile hakuna mhusika yeyote ambaye ameishatoa tamko rasmi kuwa tishio la VRF limepungua hivyo Chesi na Simba wa Tsavo wenzake ruxa kuanza kurarua nyama, ni wazi kuwa nyama zitaendelea kuning’inia kwenye mabucha kama nguo kwa dobi panoja na bei yake kupungua kuwa kwa asilimia inayosogelea mia sasa!

Waama, mpaka atakapojitokeza mhusika yoyote kumtoa wasiwasi kwa herufi kubwa kabisa, chesi ataendelea kukodolea tu macho minofu ya nyama inayoshangaa shangaa kwenye bucha huku akiendelea kuchurizikwa na mate ya umero. Alamsik.




Kuna hii fasheni mpya ambayo imeshika kasi kama moto wa nyika ya kufanyia vikao vya maandalizi ya mazishi ya mtu kwenye Bar. Nimeliandikia hili.

Kwanza, huyu wenu mpendwa alidhani hakusikia vizuri tangazo lile. Akatenga vizuri sikio lake kuukuu lililokwisha ona, kama sio kusikia, siku njema na kusikiliza tena kwa makini.

Na si kwamba alichokuwa anataka kusikia kwa ukamilifu kilikuwa ni jina la marhum, la hasha. Hilo alikuwa amelisikia vizuri na kutambua kuwa alikuwa ni mtu ambaye japo hakuwa ndugu yake, alikuwa akimfahamu vizuri. Kulikuwa na kingine kilichomvuta kusikiliza tena tangazo lile.

Na bila khiyana mtoa matangazo akarudia tena. Kwamba alikuwa anasikitika kutangaza kifo cha fulani bin fulani kilichotokea hukoo katika hospitali ya nanihii, habari ziwafikie huyu, huyo na yule wa nanihii na nanihii na mipango ya mazishi ilikuwa inafanywa kwenye baa ya nanihino!

Mipango ya mazishi inafanywa kwenye baa ya nanihii! Hiki ndicho mchangiaji wa Blogu alichodhani kuwa alikuwa hajasikia vizuri. Akawa amedhibitishiwa kwamba alichokuwa amesikia ni kweli na kwamba antena zake, kwa maana ya masikio, hazikuwa kuu kuu kiasi hicho!
Kwamba marehemu fulani bin fulani alikuwa amefariki dunia na ndugu, jamaa na marafiki walikuwa wanakutana kwenye Grosari fulani ili kupanga mipango ya kusafirisha mwili wake kwenda kuzikwa alikozaliwa. Mipango ya mazishi Bar!


Muandika katikati ya mistari na my wife wake wakakumbuka kuwa marehemu alikuwa miongoni mwa watu wachache hasa ambao ni wacha mungu kwa maana halisi tofauti na akina Chesi ambao ucha Mungu wao unaonekana zaidi siku za jumamosi kwenye harusi badala ya jumapili kwenye misa!

Haya, wakanyanyuana na kuelekea huko kwenye msiba njiani wakiulizana ni masahibu gani yaliyokuwa yameikumba nyumba ya marehemu hadi ikaamuliwe mipango ya mazishi yake ikafanyiwe kwenye baa.

Ndio, wakajiuliza maswali kibao yasiyokuwa na majibu huku kubwa kuliko yote likiwa lile la jinsi marehemu alivyokuwa mcha Mungu na jinsi atakavyokuwa anjisikia huko aliko akiangalia mipango ya kuuzika ya mwili wake ikifanyika Bar!

Tukafika pale nyumbani kwa marehemu ambapo palikuwa na liuwanja likubwa tu la kumwaga na kwa maana hiyo kuondoa dhana kwamba labda watu walikuwa wameamua kwenda kufanyia mipango ya kuusafirisha mwili wake Bar kutokana na kukosa nafasi kwenye makazi yake.

Muandika katikati ya mistari akambwaga mkuu mwenzie pale na kuelekea kule alikoambiwa ndiko mipango ya kusafirisha mwili wa marehemu na mazishi yake ilikuwa inafanyika. Nanihino Bar.
Akafika pale na kukuta ndugu, jamaa na marafiki wake kwa waume wakipanga na kupangua kipi kifanyike na kipi kisifanyike kuhusiana na msiba wa ndugu yetu huku mezani kukiwa kumesheheni vituliza majonzi’ kibao.


Kwa hakika, mtu yoyote ambaye angefika pale na kuona kilichokuwa kikiendelea, asingelaumiwa iwapo angedhani kuwa kilichokuwa kikiendelea pale ni kikao cha maandalizi ya harusi! Dhahiri angeshituka mno kuambiwa kuwa kile kilikuwa ni kikao cha maandalizi ya mazishi ya mtu!

Muandika katikati ya mistari anaomba kukiri wazi kuwa alijiunga kukaa kwenye kikao kile kwa machale huku kila mara akigeuka huku na kule akitegemea saa yoyote marehemu mcha Mungu kuwazukia pale na kuwauliza kwa kulikoni walikuwa wanafanyia Bar mipango ya kuzika mwili wake!

Ndio, kwa nini walikuwa wanafanya mipango ya kusafirisha na kuzika mwili wake kwenye eneo ambalo meza ya pembeni kulikuwa na kikao cha maandalizi ya harusi, kandokando yake kulikuwa na kikao cha maandalizi Send-off ya mtu na pembeni kulikuwa pia na kikao cha usuluhishi wa ndoa ya mtu iliyokuwa juu ya mawe!

Muandika katikati ya mistari ameishakiri mara kadhaa huko nyuma kuwa huwa huwa anafanya jitihada za za ziada kuhakikisha kuwa haachwi nyuma na anakwenda sambamba na wakati lakini karibuni mara zote amekuwa akijikuta akiachwa kwenye mataa!

Ndio, aliachwa akishangaa watu walipoanza kuvaa sare za misiba, watu walipoanza kubeba makamera ya video makaburini, watu walipoanza kuwavalisha suti marehemu wakati hawakupata kuwanunulia suti walipokuwa hai na wafiwa walipoanza kwenda saluni kabla ya shughuli ya kuaga miili ya marehemu wao.

Kwa hakika, kushangaa kwake hili lililoanza kushika kasi siku za karibuni la vikao vya mipango ya kusafirisha na mazishi ya marehemu kufanyikia kwenye kumbi za starehe linamfanya adhibitishe wazi kabisa kuwa bado yeye ni mshamba aliyepitwa na wakati. Kwa hili, anakubali aendelee kubaki hivyo.