Friday, August 24, 2007

Sasa tunatafuna nyama kama vile hakuna kesho. lakini siku chache za nyuma, gonjwa baya la Rift Valley Fever, RVF, lilifanya watafuna nyama wote waone nyama kama kituo cha Polisi. katikati ya dhahama hiyo niliandika makala hii...

Muandika katikati ya mistari anakatiza mitaani na kuangalia nyama ya ng’ombe inavyoshangaa shangaa kwenye mabucha kama vile haina mwenyewe na anaishia kujiuliza iwapo ni majuzi tu mambo yote yalipokuwa yeye na nyama, nyama na yeye.

Anaangalia jinsi minofu ya nyama ilivyobakia kuwa maeneo ya kujidai ya nzi badala ya kuwa maeneo ya kujidai ya meno yake na anaishia kujiuliza ni lini kiama hiki cha kuona nyama kama kituo cha Polisi kitakapoishia.

Waama, muandika katikati ya mistari anajiuliza mno juu ya watu hawa waliokuwa mabingwa mno wa kumtangazia na kumtaka kuiona nyama kama kibaka akionavyo kituo cha Polisi ghafla bin vuu kugeuka mabubu linapokuja suala la kumruhusu kukandamiza manyama kwa kwenda mbele.

Kwa hakika, huyu wenu mpendwa haoni aibu kukiri kwamba kama walivyo wanaume wengi wa kibongo linapokuja suala la kula nyama, yeye ni mroho plus.Ndio, kwamba linapokuja suala la supu, mishikaki, utumbo na vitengo vingine vyote vya nyama, yeye ni Simba wa Tsavo.

Ndio, kama ilivyo kwa wanaume wengi wa kibongo, yeye alikuwa ni adui nambari wani wa Ng’ombe na Mbuzi, akiteketeza bila huruma kilo juu ya kilo za nyama za wanyama hao saa ishirini na nne na siku saba za wiki.

Unaambiwa ratiba ilikuwa asubuhi kabla ya kuingia mzigoni ni supu ya ng’ombe ama Mbuzi pale mitaa ya Kisutu, mchana anafakamia wali nyama kwa mama lishe, jioni anaungana na kampani na kwenda kurarua nyama za kuchomwa na mishikaki kabla ya kumalizia nyumbani usiku wali na nyama. Naam, nyama kwa kwenda mbele!

Wakazuka hawa jamaa ambao muandika katikati ya mistari anahisi kwamba walimuona anafaidi sana na hivyo kumfanyia fitna kwa kutangaza kuwa kile alichokuwa akipenda sana kilikuwa kimeingiwa na homa ya bonde la Ufa na sasa kimekuwa tiketi tosha ya kukupeleka maeneo ya juu kwa Muumba wako.

Hakuna apendaye ku-rest in peace bila sababu za msingi. Ghafla bin vuu nyama ikageuka kuwa kituo cha Polisi mdomoni mwa muandika katikati ya mistari na Simba wa Tsavo wenzake!

Badala ya kula nyama ya Ng’ombe muandika katikati ya mistari sasa akajikuta akilazimika kula kilichokuwa chakula cha Ng’ombe, yaani majani. Kuanzia mchicha hadi kabichi hadi kisamvu hadi nyasi nyinginezo! Supu yake sasa ikawa ile ya karoti tupu!

Hapo nyuma kidogo huyu muandika katikati ya mistari alikuwa na kawaida ya kuwashangaa kwa kebehi wala mboga mboga bila nyama waliokuwa wamejipa jina la ‘vejetarian’. Akajikuta yeye sasa akigeuka kuwa vejetarian wa nguvu kuliko hata vejetarian wenyewe orijino!

Naam, kwa siku kadhaa kukawepo na taarifa za kuwataka wakazi wa jiji jema la Dizim kukaa chonjo kwa sababu homa ya ng’ombe ilikuwa hapo Boma la Ng’ombe tu, mara ikawa Dodoma, mara Morogoro, na mara Kibaha.

Kwa hakika, kuna wakati huyu Chesi alikuwa anaona kabisa kuwa magazeti yalikuwa kwenye ushindani usio rasmi wa gazeti lipi litakuwa la kwanza kuandika juu ya ugonjwa huo kuingia jijini!
RVF ikawa kushoto, kulia na katikati.
Muandika katikati ya mistari haoni aibu kukiri kwamba alikuwa akisononeka mno kuona minofu ya nyama ikizagaa zagaa tu kwenye bucha huku wanaozifaidi wakiwa mainzi tu!

Siku kadhaa baadaye muandika katikati ya mistari na waroho wa nyama wenzake anashuhudia kupungua kwa kiasi kikubwa kwa taarifa muhimu juu ya RVF. Anashangaa kuona hata ule ushindani wa vyombo vya habari wa kuandika juu ya ugonjwa huo unavyosogelea jijini ukiwa umepungua mno, kama sio kwisha kabisa.

Pamoja na upungufu huu wa taarifa za ugonjwa huo, bado muandika katikati ya mistari hajapata ujasiri wa kusimama mbele ya Bucha na kumtaka muuza nyama akamtie kiuno na kukichukua kiuno hicho hadi nyumbani kwa ajili ya kitoweo.

Naam, ameishia kuwaonea donge majasiri wanaomhadithia kuwa jana walinunua nyama na kuigagadua tani yao bila kujali cha RVF wala nini! na donge linazidi zaidi pale anapoona wagagaduaji hao wakiendelea kudunda bila hata hata dalili ya kuugua angalau kamalaria ama kamafua tu! laiti na yeye angekuwa na ujasiri huu!

Anashindwa kujidai na hilo kwa sababu hakuna mhusika yoyote miongoni mwa wale waliojitokeza kwa nguvu zao zote kumchimbia mkwara kuhusu RVF ambaye ameishajitokeza hadi sasa kutamka kuwa tishio limeishapungua hivyo mwenye kutaka kula nyama,aale. Anayetaka kula utumbo, aale. Anayetaka kukatiwa kiuno, na akatiwee!

Ndio, ni kwa vile hakuna mhusika yeyote ambaye ameishatoa tamko rasmi kuwa tishio la VRF limepungua hivyo Chesi na Simba wa Tsavo wenzake ruxa kuanza kurarua nyama, ni wazi kuwa nyama zitaendelea kuning’inia kwenye mabucha kama nguo kwa dobi panoja na bei yake kupungua kuwa kwa asilimia inayosogelea mia sasa!

Waama, mpaka atakapojitokeza mhusika yoyote kumtoa wasiwasi kwa herufi kubwa kabisa, chesi ataendelea kukodolea tu macho minofu ya nyama inayoshangaa shangaa kwenye bucha huku akiendelea kuchurizikwa na mate ya umero. Alamsik.




No comments: