Monday, July 10, 2006

kombe la dunia lina kasheshe zake. hususani kwa akina siye tunaolicheza kwa mdomo....

Kwa muda wa wiki mbili sasa, hii sehemu ambayo muandika katikati ya mistari haoni hata aibu ya kuiita ati sebule yake, imekuwa ni kijiwe ama kongamano la makocha, wachambuzi, wachambaji wataalamu na wataaluma wa soka ambao uchambuzi wao kuhusu mechi za kombe la dunia umemfanya Chizi kujiuliza kila mara watu hawa wanangoja nini hapa bongo!

Ndio, ni wataalamu na wataaluma mno wa soka kiasi kwamba nina hakika kabisa kuwa iwapo watajisumbua kidogo tu kuandika barua za maombi ya ukocha pale jiji la Manchester, basi kibarua cha mtafuna Big G mmoja aitwaye Sir Alex Ferguson kitaota magugu! hakya nani tena vile!

Halafu nimegundua pia mara nyingi kwamba utaalamu na utaaluma wa soka wa waheshimiwa hawa walio marafiki, majirani na ndugu zangu wanaokuja kukodolea macho haka katiivii kangu ka nchi kumi na mbili, huongezeka maradufu pale bi mkubwa wa nyumba na wadogo zake kadhaa wa kike wanapojiunga kuwa miongoni mwa watazamaji wa mechi husika. hapo tena, hakuna anayekubali kushindwa!

Nikagundua pia kuwa wengi wa waataluma na wataalamu wangu hawa wa soka la sebuleni walikuwa hawakuwahi kucheza japo chandimu utotoni mwao afadhali hata mimi ambaye niliishakipiga hadi ngani ya unahodha wa timu yetu ya darasa la tano mwaka 1972 pale Chang'ombe shule ya msingi!!

Naam, kwa hakika ni maoni ya wataaluma na wataalamu hawa wa kibongo yanayonifanya niamini kwamba ninachotizama sebuleni kwangu sio kombe la dunia bali soka la sebuleni la kimataifa!

Kwa mfano, kuna huyu mmoja ambaye ana shahada ya juu ya ukocha wa kuwakosoa wachezajiwa timu zinazocheza uwanjani: "Ayaa! mwangalie sasa yule migulu baja anakopeleka mpira! pale alitakiwa arudishe mpira nyuma kwa mwanangu mwenyewe Figo ama atie majalo kwa mzee mzima nanihii apige bao, badala yake anacheza mdundiko na mpira! mwangalie kwanza, jibukta kubwa kaa kisafleti!"

Ama: "Tatizo hawa Uingereza hawaijui hii infomesheni ya 3-5-2, sana sana wanalazimisha tu! pale yule Cole alitakiwa apande (sio mchicha, ndugu msomaji!) halafu huyu Ferdinand ashuke chini kama Libero, lakini waapi! ubishololo na baraka ya kuvaa mijikaptura mireeefu tu!"

Halafu yupo huyu mtaalamu mwenye shahada ya juu ya ukocha wa kuwakosoa makocha wenzake wa kombe la dunia...na hali yeye ni kocha wa sebuleni kwa chesi tu!! "Ama huyu kocha wa Uruguay ndio amepanga timu gani sasa hii! hawa lazima leo wapigwe bao tu! pale alitakiwa amtoe yule namba kumi na moja ambae anazunguka tu uwanjani kaa daladala na sio amtoe yule namba tisa ambaye mambo makubwa yake tunayaona! mii nakwambia hawa makoccha wengine basi tu! muone kwanza, suruali kaa yangu!!"

Alikuwepo pia mkereketwa mmoja aliyekuwa akiiona Ghana kama ni mkoa wa.. waaa... wa..ah, sijui wa ngapi vile wa bongo; "Angalieni wanaume hao! mi nakwambieni hawa ndio mabingwa wapya wa dunia mwaka huu! Si unaona mwenyewe alivyomtungua bao mbili kwa gurudumu yule mcheki?

Yatosha tu kusema kwamba baada ya Ghana kufungishwa virago, mkereketwa huyu hatukumuona tena kwenye uwanja wetu wa sebuleni na kwa kweli tukaukosa mno utaalamu wake mkubwa katika soka la kimataifa, hususani ilipokuja suala la 'mkoa' wake wa Ghana!

Alikuwepo pia huyu bwana mdogo wangu mmoja ambaye yeye alikuwa na kazi moja tu ya kufananisha mambo: "Ebwanaee! umecheki darizi lile la mzee Patrick Viera! Duh! yaani kama lile lile alilofanya yule nanihii wa wekundu wa Msimbazi kwenye ile mechi kati ya nanihii na nanihii pale uwanja wa taifa!"

Au: "Duh! Ebwanaee! hii midfield ya Ureno mwanangu sio mchezo! inagawa mavyumba na mapande kama anavyogawaga Nanihino wa Wanjano wa Jangwani! yaani, wee acha tu!"

Step fulani bwana mdogo wangu huyu katika kujaribu kwake kujijazia maujiko kwa mabinti zangu, akajaribu hata kufananisha viwanja: "Dah! lile jukwaa la uwanja wa Munich sio mchezo, mwanangu mwenyewe! Yaani, dah! kaa lile dude letu la Kirumba!"

Kauli hii ikaufanya uzalendo wa watazamaji walio wengi uyeyuke. wakamtaka bwaa mdogo wangu yule afunge bakuli lake, ama aende akalale na awaachie watu waangalie mpira. akakubali kufunga bakuli. nahisi alikuwa hana hata kitanda.

Alikuwepo pia mtaalamu wa kukandya: "Mii nawaambia hizi timu nyingine sijui hata zinafikaje kwenye fainali hizi, kama sio kubebwa tu! mtu utafungwaje gongo sita, bwana? ee? mtu utafungwaje gongo sita kaa umesimama! mi nawaambia hata taifa stars yetu ingepeta kichizi kwenye fainali hizi!"

Hata hivyo mtaaluma huyu akashindwa kutufafanulia ni kwa vipi basi hio Taifa stars yetu haijafanikiwa hata kunusa tu huko kwenye watu wanaopigwa gongo sita kaa wamesimama, na hali yenyewe ingepeta tu kwa sana!

Kipindi fulani, hata huyu bi mkubwa wa nyumba naye pia akataka kuonyesha kwamba hayuko nyuma katika mambo ya kandanda na kwamba akiamua kujisumbua kidogo tu kwenda Uingereza kutafuta kazi ya ukocha, kibarua cha mfaransa Arsene Wenge kitaota mbawa: "Yule kocha naye mbona amezubaa hivyo, kaa mkono wa kanzu! si anatakiwa awaambie wachezaji wake kwamba kila pale mwenzao anapopiga penati(akimaanisha kona!) wao waende wakamvamie kipa na kumsukuma ili wafunge goli!"

Ni ajabu kwamba pamoja na wataalamu na wataaluma kibao wa soka waliojazana sebuleni mwangu mule hakuna hata mmoja aliyediriki kuinua mdomo wake na kumsahihisha bi mkubwa wa nyumba kwamba kilichokuwa kikipigwa ni kona na wala sio penati! hakukuwa na mwenye jeuri hio.

Kiboko cha wote hata hivyo alikuwa huyu lastborn wangu wa miaka saba, mheshimiwa sana Desi. wakati wenzake tukiendelea kuangalia mpira yeye alikuwa akiendelea na michezo yake mingine. pale goli lilipoingia ndipo alipokuja mbio na kutaka kujua...ni rangi gani ambayo imefunga!

Naam, yeye alichokuwa anamaindi ni rangi tu, hayo mambo ya sijui Ghana, sijui Brazili ama Uingereza ama Trinidadi na Tumbaku alituachia tujaze wenyewe!!

Yote kwa yote, katika kipindi hiki kigumu ambacho kila kitu kimepanda bei, wataalamu na wataaluma hawa wa soka la kimataifa , kupitia tiivii ya nchi kumi na mbili iliyo kwenye sebule langu, wananipa angalau sababu ya kutabasamu!! jumapili njema ya kushabikia wenzetu!

No comments: