Tuesday, February 06, 2007

..Kuna huu mchezo ambao katika siku za karibuni umeshika kasi sana miongoni mwa wabongo. kufukuza kuku. sikubaliani nao...

Kwa sisi ambao tulizaliwa 'mitaa' ya mwaka 47, kuku ni miongoni mwa viumbe muhimu kabisa vilivyoumbwa na Muumba wetu na vinavyopaswa kuheshimiwa na kuenziwa kwa nguvu zetu zote.
Naomba kuharakisha kufafanua kabisa hapa kwamba ninapozungumzia kuku ninazungumzia kuku kwa maana halisi ya kuku na sio hii mizoga inayochinjiwa nchi fulani ya mbali mwezi wa tisa na kuja kuuzwa hapa mwezi wa kumi na mbili.

Ndio, sizungumzii hawa kuku wenu wa kisiku hizi ambao ukiingia kwenye banda ukikuta mmoja ni mwekundu basi ni wote ni wekundu kama vile wamevaa sare ya shule tofauti kabisa na wale kuku wetu ambao kuku moja anaweza kuwa na rangi arobaini kidogo, kahawia, njano, nyekundu na hata bluu ili mradi kwa raha zako...!

No. ninapozungumzia kuku nina maana ya yule kuku ambae anajua kubangaiza mwenyewe kutafuta msosi na chochote kinachokatisha mbele ya mdomo wake basi ni halali na ni msosi tosha. iwe ni jongoo, gololi, vigae vya chupa, mkaa, kinyesi cha binadamu na hata cha kwake mwenyewe, vyoote ni mbele kwa mbele!

Nazungumzia yule kuku ambaye kwa kawaida kule vijijini tunakotoka, kuchinjwakwake, ikianzia pale watu wanapoanza kunoa kisu ambacho kabla ya hapo kazi yake kuu ilikuwa ile ya kumenyea viazi vikuu, ndizi na mihogo ndio alama kuu ya kuwa nyumba fulani imefikiwa na wageni!
Nazungumzia yule kuku ambaye anapoona masanduku yakiingia tu kwenye nyumba kuashiria mgeni machale yanamcheza na anatoweka haraka kwenye maeneo jirani hadi pale mkuu wa nyumba anapotoa amri ya kumkamata na kumchinja kuku mwingine anayeshangaa shangaa wakati wenzake wameingia mitini kuepuka kuwa kitoweo cha mgeni!

Aha! namzungumzia kuku wa kienyeji ambaye ili kupata mnofu wake ni lazima mdomo wako na mkono wako kwanza vicheze mchezo usikokuwa na tofauti sana na mchezo wa kuvutana kamba. kutafuna mfupa? sahau. labda kama huna haja tena na taya lako!

Naam, namzungumzia huyu kuku wa kibantu ambaye mwanzoni kabisa mwa miaka ya sitini wakati makamasi yakiwa kitambulisho muhimu na cha kudumu usoni mwangu, marehemu mzee Mpilipili alikuwa nao kama alfu tatu ama nne hivi waliomfanya kuwa miongoni mwa wafugaji wa nguvu sana wa kuku mitaa ya huko usambaani enzi hizoo.

Na wakawa ni kuku hawa hawa ambao stepu fulani wakapitiwa na kombora lililokuwa likijulikana enzi hizo kama kideri ama mdondo ambapo walianza kufa kwa mamia yao kama hawana akili nzuri vile.

Ikamlazimu Mzee Mpilipili kutoa ruksa ya kumshughulikia kuku yeyote aliyeonekana kusinzia sinzia kulikokuwa ndio dalili ya kupatwa na kideri. ruksa ikawa imepewa watu ambao hawapigiwi wanacheza, sembuse wakipigiwa. ikawa ni mauaji ya kimbari ya kuku.

Unaambiwa mambo yote yakawa ni kuku 24 hours. Tena bila mrija, mwanangu. asubuhi kuku kwa uji. mchana kuku kwa makande na usiku kuku kwa Bada. hujui bada? Pole. tafuta rafiki yako wa kisambaa akujuze. ndipo utakapojua kuwa kuna vitu vyeusi kabisa kuliko giza ulimwenguni humu!

Pamoja na yote hayo, bado mzee Mpilipili aliendelea kuwa na kawaida ya kutusisitizia kumuheshimu kuku na mnyama mwingine yoyote kwani kila mnyama alistahili heshima. kwamba hata kule kubeba mifupa iliyokwanguliwa vyema na vinjino vyetu na kwenda kuwaringishia watoto wenzetu haikuwa imetulia na ilikuwa ni sawa na kuchezea chakula.

Naam, ndivyo tulivyokuzwa na tukakua tukiamini kwamba kweli, kila kiumbe kilichoumbwa na Muumba kilistahili heshima hata kama kilikuwa ni kitoweo tu.

Kwa bahati mbaya kabisa, katika siku za karibuni ama kwa kisingizio cha siku zote cha kwenda na wakati ama kwa kukosa busara tu, muandika katikati ya misatri anashuhudia kile ambacho kwa mzee Mpilipili kisingekuwa pungufu ya kuchezea chakula.

Muandika katikati ya mistari anashitushwa na kushangazwa na tabia iliyoshika kasi ya kuku kugeuzwa kuwa ni kifaa cha michezo kama ilivyo kwa mpira ama nyavu za magoli. anashangaa kuona kila watu wanapokusanyika kwa sherehe hii ama ile, miongoni mwa michezo inayopewa chati kwa sana unakuwa ule kufukuza kuku!

Tena basi afadhali mchezo wenyewe ungekuwa unafanywa na na watoto wadogo, sivyo. muandika katikati ya mistari anaachwa hoi kabisa pale anaposhuhudia mijitu mizima na mavitambi yao, sijui akili, eti yakifukuzana na kuku!

Yaani kukimbia na gunia ama na chupa kichwani ama na kijiko chenye yai mdomoni sasa si michezo tosha tena hadi watu wazima na fahamu zao wamtese kuku kwa kumfukuza huku na huko na kumfanya atoe ulimi nje huku wafukuzaji na mavitambi yao wakihema na kutoa ulimi nje maradufu! kwa hakika ni bahati yao tu kuwa kile chama cha kutetea haki za wanyama sasa kimebaki herufi kubwa tu!

Marehemu mzee Mpilipili alikuwa hakopeshi kusema ni kuchezea chakula pale alipomuona mtu anaviringisha tonge zaidi ya mara tatu nne zilizotakiwa ili kuliweka katika hali nzuri ya kupita kooni. mi mwanayenaamini kuwa kufukuza kuku kama aina fulani ya mchezo hakuna tofauti yoyote na kuchezea chakula. nawakilisha.

No comments: