Thursday, April 27, 2006

chesimpilipili

kuna hii ambayo inawahusu hawa waheshimiwa wanaotutunzia vi-akiba vyetu vya uzeeni......




Kwa hesabu za haraka haraka, huyu mwanaGlobu mpya atatimiza birthday yake ya sitini mnamo mwaka 2019, miaka michache sana kumi na mbili tu ijayo.

Huo ndio mwaka ambao hawa watu wanaomtunzia vijisenti vyake vya uzeeni wamemuambia kwamba ndio ataweza kuchukua kilicho chake, kwa maana ya hatimaye kulia kivulini baada ya miaka kibao ya kuchumia juani.

Kwa jinsi kazi ya kuuza kila kilicho chetu ilivyoshika kasi na hao wanaovinunua wanavyotustaafisha kushoto, kulia na katikati kama vile hawana akili nzuri, Chesi ana uhakika kwamba kufikia mwaka huo wa 2019 yeye atakuwa aliishastaafishwa kazi miaka miaka kumi na nne kabla, yaani mwaka 2008.

Atakuwa ameachishwa kazi mwaka huo wa 2008 akiwa dogo wa miaka 49 tu, lakini kutokana na hii sheria ambayo kwa hakika inaweza kupitishwa nchi kama ya bongo tu, atakuwa amezuiwa kuchukua chake ati mpaka afikishe miaka sitini, yaani huoo mwaka wa 2019! mungu wangu!

Ndio, kwa hakika hii ni sheria ambayo inaweza ikapitishwa nchi kama ya bongo tu! yaani mtu ufanye kazi miaka thelathini, ustaafishwe ukiwa na miaka hamsini halafu mtu akuambie huwezi kuchukua akiba yako mpaka utakapofikisha miaka sitini!

MwanaGlobu anajiuliza kama sheria hii ingepitishwa iwapo hawa walioipitisha nao wangeambiwa hawawezi kuvuta kiinua mgongo chao cha milioni thelathini na kitu,(baada ya 'kufanya kazi' kwa miaka mitano tu) hadi pale na wao watakapofikisha miaka 60, hapana,80, kutokana na ukweli kwamba wengi wao tayari wako kwenye anga za miaka 60!!!

Thubutu kama sheria hii ingeona jua la nje!

Haya, kwa rehema za Mungu huyu mwanaGlobu anafanikiwa kufikisha miaka yake sitini. bila shaka atakuwa amejichimbia huko kwao Bumbuli, kutokana na ukweli kwamba baada ya kustaafishwa kazi, hakuwa na jeuri yoyote ya kuendelea kubanana hapa hapa mjini kama wenzake!

Atafikisha miaka yake sitini na atajikongoja kutoka huko kwao na kuliingia jiji la Dizim la mwaka 2019. labda wakati huo stend ya mabasi itakuwa Kibaha. Pengine pale mtaa wa Samora jengo fupi kuliko yote litakuwa la tughorofa thelathini. mengine yote yatakuwa mawinguni.

Anaweza pia akakuta hata ile sanamu ya askari pale imebinafsishwa na mwekezaji kuamua kuivunja na kuweka kijifast food cha nguvu katikati ya ule mzunguko! hakuna kisichowezekana Bongo.

Na ni kutokana na wingi wa majengo mareeeefu, ndio maana pengine Chesi atapata tabu sana kulipata jengo ambalo lilikuwa ndio makao makuu ya shirika ambalo lilikuwa linamtunzia visenti vyake hadi atakapofikisha miaka 60.

Ni hatimaye sana, na baada ya kuzunguka mno ndipo pengine Chesi atabahatisha kuliona jengo hilo nje kabisa ya mji likiwa na tugorofa thelathini tu! bila shaka nje ya mji wakati huo itakuwa kibaha maili moja!

Ataingia mapokezi na kumkuta huyu binti ambaye bila shaka bibi yake mzaa mama alifanya kazi na chesi miaka hio, sio ofisi moja bali kwa rika.

Na kwa vile pengine enzi hizo watu watakuwa bize sana zaidi ya ilivyo sasa, binti yule hatapoteza muda kumuamkia kizee Chesi na moja kwa moja: "sema shida yako, wee mzee!"

Chesi ataeleza shida yake, kwamba amekuja kuchukua masimbi yake kwa vile amefikisha miaka sitini. binti atamuelekeza chesi kwa ofisi husika. atamuelekeza, huku macho yake 'yakiuliza' wazi kabisa inakuwaje mpaka siku ile chesi awe bado anapeta tu wakati vizee vyenzake vimeishauona ufalme wa mbingu kitambo!

Haya, chesi anapanda gorofa ya kumi na saba kwa muhusika ambaye anamuelekeza gorofa ya tatu kwa muhusika ambaye anamuelekeza gorofa ya saba kwa nuhusika ambaye anamuelekeza gorofa ya kumi na nane kwa muhusika mwingine na mwingine tena. mpaka hapa, mambo kwa Babu Chesi ni kizunguzungu kitupu!

Hatimaaaye, anampata huyu muhusika ambaye anamfahamisha Babu Chesi kwamba Ofisi yake haina kumbukumbu zozote zinazohusu kampuni aliyokuwa akidundia mzigo chesi, hivyo... chesi alie tu....! na labda miaka hio msemo utakuwa....chesi acheke tu!

Na kweli, chesi anatamani kulia na kucheka kwa pamoja. Yaani baada ya kusubiri kwa miaka kumi na tatu mizima baada ya kustaafu, leo hii anaambiwa hana chake!kwa hakika ni jambo la kushukuru kwamba haanguki na kufaint na kufariki pale pale kutokana na mshituko!

Huyu mhusika wa mwisho angalau anaonyesha kutaka kumsaidia chesi kadri ya uwezo wake,hususani baada ya kutamka kwamba "alaa! kumbe wewe ndio mzee chesi mpilipili! mama huwa ananihadithia kwamba alipokuwa kijana alikuwa akipenda sana kusoma makala za mwindishi mmoja aliyekuwa akiitwa chesi mpilipili! kumbe ndio weewee!"

Kijana yule anamsaidia chesi kwa kupanda gorofa hili na kushukia lile, kuingia ofisi hii na kutokea ile na kufungua disketi hii na CD ile, lakini waaapi. mwisho wa yote hakuna rekodi yoyote inayopatikana kuonyesha kwamba chesi anapaswa kulipwa masimbi yake wakati atakapofikisha miaka sitini!

"unajua, mzee chesi, hapa katikati tumehama hama sana kiasi kwamba bila shaka baadhi ya nyaraka zetu zitakuwa zimemisiplesiwa na tarakilishi zetu zimekrashi !"

"eniwei, wee njoo tena baada ya miezi sita na nitaangalia ni vipi!ninaweza kukusaidia! napenda kukufahamisha pia kwamba mama atafurahi sana leo nikimfahamisha kwamba nimekutana na mzee chesi!" kijana anatoa tamati na mchezo unaishia hapo.

chesi anaondoka jijini kipara na kurudi kijijini Bumbuli akiwa amezeeka ghafla na kuonekana ni kizee wa miaka 85 badala ya 60 aliyonayo. anazeeka zaidi anapokumbuka kwamba kijijini aliondoka kwa mkwara mzito kwamba atakaporudi kutoka mjini, watu watajua yeye ni nani!

Naam, ni kwa mlolongo huu wa mawazo ndio maana chesi anadhani kwamba anapostaafishwa ni afadhali akamilishiwe chake kabisa aangaze mbele, na kama kuna kasoro katika rekodi zake, aweze kuzishughulikia akiwa bado na nguvu zake.

Ndio, hii 'bahati nasibu' ya kusubiri hadi afikishe miaka sitini, potelea mbali kwamba ni hapo kwenye kona tu, ndipo aambiwe ahana chake yeye haafikiani nayo.

vinginevyo, hata wale walioipitisha sheria hii ya ajabu nao wanapomaliza miaka yao mitano ya kudunda mzigo, waambiwe kiinua mgongo cha cha milionizao 30 watalipwa pale watakapofikisha miaka 80, kwa mantiki ile ile kwamba wengi wao tayari wapo kwenye anga za miaka 60, tuone kama watakubali! nawakilisha.

2 comments:

Ndesanjo Macha said...

Kweli tulikuwa tunakosa uhondo sana kwa kutokusoma muda mrefu (ninamaanisha wale walioko nje ya Tanzania). Sasa tunaburudika. Nacheka sana ila najua unayoongelea sio mzaha. Nitarudi hapa tena na tena na tena.

Kuhusu kiinua mgongo, kwanini usijaribu pale gorofa ya 17? Kama faili limeliwa na panya, basi nenda gorofa ya 22 kwa bosi ambaye itabidi umwendee kwa miaka miwili kabla ya kupata wasaa wa kumuona!

Chesi said...

asante ndesanjo. nitajaribu kufanya hivyo huku nikiomba Mungu kuwa siku hiyo lifti inafanya kazi......!!